Kurasa

Tofauti ya Ubia na Uwakala kisheria.


Waziri wa Katiba na Sheria, Dk.Asha-Rose Migiro.
Ubia na Uwakala ni maneno tunayotumia sana katika jamii zetu, ila si wote wanaofahamu hasa yana maana gani. Ndiyo maana basi, mara kwa mara tu basi watumiaji wengi wa maneno haya huyachanganya kwa kusema ubia pale  ilipopaswa kuandikwa ama kutamkwa uwakala, na kinyume chake.
 
Kwa hivyo basi, nitumie fursa hii hapa kuzitofautisha dhana hizi mbili yaani ubia na uwakala. Ufafanuzi unaotolewa hapa unaweza kutokidhi kiu ya mwanazuoni wa lugha, kwa vile nayafafanua maneno haya kwa vile yanavyoeleweka kisheria.
 
Kisheria mambo yote mawili, yaani ubia na mkataba, ni mahusiano yanayoangukia katika sheria za mikataba ingawa wasomi mahiri walioyachimba mambo haya kwa kina zaidi (kama alivyo Mwingereza Lindley, kinara wa sheria za Ubia) wameweza kuvifanya vipengele hivi kuanza kuonekana kama vinavyojitegemea kutokana na utata utokeao ndani ya mambo haya ya ubia na uwakala. Kwa hivyo basi, iwapo tunafuata utaratibu huu basi, Sheria ya Ubia huitwa Partnership Law (kimombo) wakati ile ya Uwakala inaitwa Agency Law.
 
 Kwa hapa Tanzania, Sheria ya Mikataba ambayo ni Sura ya 345 ya Sheria za nchi inazifafanua dhana hizi kirefu. 
 
Sheria hii ya mwaka 2002 haina tofauti sana na ile ya awali ya mwaka 1961, isipokuwa imeyaweka bayana zaidi masuala yaliyokuwa yakileta utata ndani ya sheria hii, kati ya mwaka 1961 hadi 2002 sheria zetu nyingi zilivyohakikiwa tena, ambapo sasa hata zile tafsiri za sheria ya awali, kama zilivyotolewa na Mahakama Kuu na ile ya Rufaa pamoja zimezingatiwa kwa kuingizwa au kukataliwa.
 
Uwakala (Agency) umefafanuliwa katika Sehemu 10 ya Sheria hii, wakati ambapo Ubia (partnership) umewekewa misingi yake na kufafanuliwa kisheria katika sehemu ya 11 ya Sheria hiyo hiyo. 
 
Kwa ujumla wake, ukivisoma vifungu vyote 54 (kuanzia kifungu cha 134-189) ambavyo vinajikita katika kufafanua maana, haki na wajibu wa wahusika katika masuala ya Uwakala  kisha ukavilinganisha na vifungu vyote 36 (yaani kuanzia kifungu cha 190-226) huku ukizingatia misingi na sheria nyinginezo, basi mambo haya yafuatayo yanaweza kubainishwa kuhusu kushabihiana (kufanana) au kutofautiana kwa ubia na uwakala:
 
(1)Ubia na Uwakala, vyote viwili vinaangukia katika sheria za mikataba. Kwa maana hii basi, unapohitajika ufafanuzi Sheria za mikataba zinatumika zaidi.
 
(2)Ubia (partnership) unafanana na uwakala (agency) kwa kuwepo zaidi ya mtu mmoja katika kufanikisha hicho kinachofanyika ama kukusudia kufanyika. Bila watu wawili ama zaidi hakuna ubia na bila watu wawili au zaidi hakuna uwakala pia. Huwezi kufanya ubia peke yako na huwezi kufanya uwakala peke yako. Kwa ufasaha zaidi ni kuwa mtu mmoja pekee anaweza kufanya biashara anamiliki pekee lakini atahitaji mtu au wengine zaidi kufanya ubia au uwakala uwepo.
 
(3)Tofauti kubwa ya ubia na uwakala ni kuwa katika ubia wahusika wanakubaliana kufanya jambo kwa pamoja, wakizingatia mchango wa pamoja, kugawana faida, hasara na kadhalika lakini kwenye uwakala, kitu hiki hakipo kwa sababu muuza vocha anayeuza vocha za kampuni fulani ya simu (vodacom, tigo, Airtel, Zantel, Ttcl na kadhalika) yeye ataendelea kidunduliza faida hata kama hukuwa na ubia na kampuni ambayo anauza vocha zake imeingia hasara kubwa kama kampuni. 
 
Yeye hakimgusi kwa sababu si mmliki (mwanahisa) na wala hana kitu cha pamoja kinachowaunganisha kama daraja (kwa maana ya ubia sasa) na kampuni hiyo.Hasara wangegawana ubia kama upo. 
 
Mfano wa hapa ni kampuni ya magari ya TOYOTA iingie ubia wa kutumia matairi ya MICHELIN na yakishauzwa wagawane faida. 
 
Iwapo inatokea magari ambayo yangeuzwa yanapata hasara, wote wawili hawa watapata hasara na iwapo watauza na kupata faida basi wawili wanafaika na faida hiyo kama wabia.
 
(4)Katika ubia wahusika wanaweza kuwa na hadhi na nguvu zinazofanana au kukaribiana na pengine wajibu, haki na maslahi yanayolingana au kutofautiana kidogo (japo mara chache yakawa na tofauti kubwa pia) lakini katika uwakala kuna mkubwa na mdogo. 
 
Katika uwakala mkubwa mara nyingi ndiyo hupanga nini kifanywe na yule anayetoa huduma kama kuuza  bidhaa au kutoka huduma kwa niaba yake. Mara kwa mara huyu mkubwa (Principal) hupanga nini kifanyike na hutoa sharti ambalo mdogo huwa na nafasi finyu ya kukikataa anachoelekezwa. Mfano ni mawakala wa LUKU za TANESCO au wauza vocha ama huduma za kifedha za makampuni ya simu kama M-PESA. Hawa hutekeleza kile ambacho mkubwa anawaagiza na si rahisi wakala anayeuza kadi za simu kutaka apangiwe au auze bidhaa bei tofauti na iliyopangwa juu. 
 
Baada ya kuliona hili tusifikiri sasa kuwa, wakala hana haki. Wakala ana haki kama ambavyo alivyo na wajibu kwa mkubwa wake. Hivyo hivyo, mkubwa (Principal) ana haki zake kisheria kama alivyo na wajibu.
 
Sheria ya Mikataba (Sura ya 345) inaelezea wajibu alionao kwa wakala wake. Mathalani, kifungu cha 174 kinampa haki wakala kufidiwa katika jambo ambalo limemfanya aingie hasara iwapo jambo hilo alilifanya kihalali na kwa mujibu wa sheria. 
 
Iwapo, sheria inaelekeza wakala wa kutoa mizigo bandarini afanye mambo na akayatekeleza kama sheria na utaratibu unavyoagiza na akaingia hasara. Basi aweza kulipwa fidia kama ambavyo wakala wa kutoa fedha kibenki anatekeleza sheria ya kutoa fedha kwa niaba ya taasisi fulani na kukatokea akaingia hasara. 
 
Kifungu cha 175 kinamlinda pia iwapo anaingia, lakini akafanya jambo fulani likamfanya aingie hasara kama atathibitisha kulifanya kwa nia njema. 
 
Masuala haya hutegemea ushahidi na kila kesi ni tofauti na nyingine  ni vema kupata msaada wa mwanasheria kwa uhakika.
 
*Denis Maringo ni mwanasheria aliyeko Dar es Salaam. Mawasiliano: dnmaringo@gmail.com (barua-pepe) na 0719270067 (simu). 
CHANZO: NIPASHE